Boom Focus | Tunamtazama Mr Blue
Heri Sameer Rajab maarufu kama Mr. Blue ndiyo msanii ambaye tunamtazama katika Boom Focus siku hii ya leo.
Staa huyu ni kioo halisi cha muziki wa Bongo Fleva. Alizaliwa Aprili 14, 1987. Matamanio yake ya kufanya muziki yalianza tangu akiwa kijana mdogo wakati huo akisoma elimu ya msingi.
Kwa mujibu wa vyanzo kadhaa, miongoni mwa watu wa kwanza kumfungulia milango ya kufanya muziki ni Abby Skills ambapo mwaka 2003 kuelekea 2004 alifanikiwa kuachia ngoma yake ya kwanza kabisa 'Blue Blue' ambayo ilimpatia umaarufu mkubwa na kumpa nafasi ya kufahamika kwa wapenzi wengi wa muziki nchini Tanzania wakati huo.
Baada ya ngoma hiyo hakupoa na aliamua kuachia ngoma nyingine 'Mapozi Nami'. Kuanzia hapo akashika kasi kubwa na kujizolea umaarufu mkubwa na kupata mashabiki wengi sana.
Amewahi kupitia misukosuko kadhaa na kuamua kukaa kimya bila kuachia ngoma yoyote kuanzia mwaka 2011 mpaka 2013 kutokana na kifo cha mama yake ambapo alihisi ametengwa na dunia kutokana na umuhimu mkubwa aliokuwa nao mama yake kwake.
Baadaye alikaa sawa na kuachia ngoma nyingi kali kama vile 'Pesa', 'Tabasamu', 'Siwezi', 'Mbwa Koko', 'Mboga Saba', 'Baki Na Mimi', 'Natutaki', 'Raha' na nyingine nyingi.
Vile vile wasanii kadha wa kadhaa wakiwemo wenye majina makubwa kwa sasa wakati wanaanza muziki wamefanikiwa walau kidogo kupita kwenye mikono yake kama vile Alikiba, Diamond Platnumz na wengine wengi.
Miongoni mwa kolabo kali ambazo amewahi kufanya ni ngoma ya 'Nilikitaa' ambayo alishirikiana na TID na Q Chilla wakati huo wakiunda Kundi lao lililojipatia umaarufu mkubwa la 'Top Band'.
Kolabo nyingine ni 'Dhahabu' alioshirikishwa na Dully Sykes, ambapo pia alikuwepo Joselin. Ni moja ya ngoma ambazo zilitamba sana wakati huo.
Upekee mkubwa alionao Mr Blue ni uwezo wake mkubwa wa kuimba pamoja na ku-rap, na vyote akivifanya kwa umahiri mkubwa sana.
Kwa sasa anatamba na ngoma yake 'Baby Boo' ambao ameuachia siku chache zilizopita akiwashirikisha Ibraah & Baddest 47 na unapatikana Boomplay. Endelea kusikiliza 'Baby Boo' hapo chini kupitia Boomplay.
Baby Boo ft. Ibraah & Baddest 47
#BuzzBrandColumn #BoomFocus #Music #MrBlue #Trending